Friday 16 October 2015

For reference: Tushikamane overview - Kiswahili

EMBRACE – Tushikamane:
Kupunguza vifo kupitia uhamasishaji jamii na vikundi vya wanawake

                              
Mradi wa Tushikamane unalenga ‘Kupunguza vifo wakati wa ujauzito na utotoni’


Jina la Mradi kwa Kiingereza ni EMBRACE kifupisho cha
‘ Empowering Mothers and Babies to Receive Adequate Care & Equality’
Maana yake: Kuwawezesha Akinamama na Watoto Wachanga kupata
 Matunzo ya Kutosha, na Usawa
Kusudio la Mradi:
Kupitia uwezeshaji na elimu kwa wanawake, Mradi unatarajia kupunguza vifo vinavyoweza kuepukika, na kuleta ahueni endelevu  inayogusa nyanja mbalimbali  za maisha ya watu wenye hali duni waishio vijijini Tanzania.


Tatizo: Vifo vya kushitikisha vya wanawake na watoto wachanga  sehemu za vijijini Tanzania.

Mwaka 2013, kote duniani, jumla ya wanawake  289,000 walipoteza maisha kutokana na matatizo yanayohusiana na ujauzito na kujifungua.  Kwa kila mwanamke mmoja anayepoteza maisha, takiriban wanawake wengine 20 hupatwa na majeraha makubwa, maambukizi au ulemavu.

Maeneo mengi ya Tanzania vijijini hukumbwa na matukio mengi haya ya kusikitisha ambayo yangeweza kuepukika:  Kila siku, wanawake 35 hufariki kutokana na sababu zinazohusiana na kujifungua. Katika maeneo ya vijijini, mtoto 1 kati ya watoto 10 hufariki kabla ya kutimiza miaka 5. Idadi isiyojulikana hupatwa na madhara mengi mabaya kama vile  kuharibika ubongo. 

Katika maeneo ya vijijini  ambayo hayafikiki kwa urahisi  kama vile  Tunguli, kwa ukweli, karibia mwanamke  1 kati ya  100 hufariki wakati wa kujifungua. Sababu 5 kuu za vifo hivyo zinaweza kudhibitiwa: kupoteza damu nyingi, sumu kutokana na maambukizi kuenea kwenye damu (sepsisi), mtoto kukwama kutoka, kifafa cha mimba, na utoaji mimba kwa njia zisizo salama.  Kila kifo cha mama ni pigo kubwa kwa kijiji chake kizima – nani atawalea watoto wake wengine, na kuhangaika na majukumu mengine ya kimaisha ya kila siku  ?

Kuna sababu nyingi zinazoingiliana  ambazo huchangia  matatizo haya ya msingi kutoshughulikiwa ipasavyo, kwa mfano: kutopata huduma za afya; ukosefu wa usawa kijamii; kukosa elimu; magonjwa yasiyopona ; utapiamlo; mgonjwa kutakiwa kusafiri mbali kupata huduma; kutozingatia uzazi wa mpango; na huduma duni za usafiri. Mzizi wa haya yote ni kwamba asilimia 90 ya idadi ya watu wote huishi kwa  kipato cha dola 2 (Shs 4,200/-) kwa siku au chini yake.

Hospitali ya Berega  huhudumia  eneo kubwa  lisilofikika kwa urahisi Tanzania vijijini lenye watu takriban 217,000. Kuna vizazi 8,500 kwa mwaka, ambapo  watoto 1,000 tu ndio huzaliwa kwenye kituo cha afya. Kituo cha afya cha Tunguli huhudumia eneo lenye mraba karibia kilomita  625 na kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2012, eneo hii linaweza kujumuisha watu 20,000, (ingawa siyo wote hutumia ipasavyo huduma za Kituo cha Afya cha Tunguli ).




Kwa nini tuanze  kwa  kuihamasisha  jamii na vikundi vya wanawake ?
Kwa nini tusiende kwenye matatizo moja kwa moja ?!


Katika kushughulikia jambo lenye kuhitaji ufumbuzi wa haraka, unaweza kushawishika kutoa ufumbuzi wa moja  kwa moja –mathalan kujenga zahanati, kuanzisha kiliniki ya uzazi wa mpango, kutengeneza miundombinu nk. Kutoa ufumbuzi wa moja kwa moja ndiyo njia sahihi ya kufanya, ili mradi ufumbuzi huo uwashirikishe wanajamii, na ili mradi kuwepo na shinikizo au msukumo wa muda mrefu wa kuboresha hali husika. Hata hivyo, ukweli usiofurahisha ni kwamba kawaida Barani Afrika, jitihada za ufumbuzi mara nyingi hufanyika bila kuwashirikisha wanajamii ipasavyo, na mara nyingi hakuna makakati wa muda mrefu wa ufuatiliaji baada ya hapo. Juhudi kama hizi mara nyingi husuasua, na kawaida hushindwa kupunguza vifo: vifaatiba huharibika; mbinu bora mpya  za utendaji  hazizingatiwi, watu hushindwa  kuhudhuria; na zana  hukosa matunzo nk.

Hasa kuhusiana na ufumbuzi unaotokana na  misaada ya wafadhili wa nje, kama jamii hazioni  miradi au huduma hizo kuwa zao, basi zinakuwa hazijalenga vipaumbele kwa usahihi.  Hakika, vigezo muhimu ambavyo huchochea  vifo vya mama na watoto vimegemea  kwenye tabia za wale ambao  mara nyingi sauti zao  hazisikiki vya kutosha  katika maamuzi: wanawake  – mathalan  katika kutafuta huduma za uzazi wa mpango, huduma za uzazi hospitalini, au chanjo; matumizi ya maji safi na salama na vyandarua; kuendelea na unyonyeshaji; uelewa wa lishe bora  kwa  watoto; kutambua magonjwa hatari; nk. Katika kaya ambazo bado zimegubikwa sana na   mfumo dume, wanaume wanaweza kutoelewa fika vipaumbele muhimu katika  kuokoa maisha ya mama na watoto.


Kama kinachohitajika kubadilishwa ni tabia za wanawake walio katika umri wa uzazi, ufumbuzi siyo  wageni au wafadhili kutoka  nje kuja na kuwambia nini cha kufanya.  Njia sahihi  ni kuanza na kutoa elimu na  kujenga uelewa, lakini kwa njia ambayo inatengeneza  wanawake   mifano  ndani ya jamii husika, ili wanawake wengine  waweze  kuiga kutoka kwao tabia na utendaji  ambavyo vinaweza kuchangia kuepusha vifo. Wanawake wanapaswa kuwa na sauti kubwa zaidi.

Sauti kubwa ya wanawake, baadae, itachangia  utambuzi wa mahitaji mengi ya msingi  kama vile usafiri, uzalishaji shambani, ajira, maji, chakula, upatikanaji wa huduma za afya za msingi nk. Kushughulikia mahitaji haya ya msingi, baada ya jamii kuyabaini kama mahitaji yao na kuyapa kipaumbele, kutachangia  miradi au huduma  zitakazoanzishwa  kufanikiwa.  

Kutokana na ushahidi katika nchi kadhaa, ni wazi kuwa njia bora ya kufanya kazi na wanawake walio katika umri wa uzazi  ni kupitia vikundi vya wanawake kwenye jamii  zao. Ingawa vikundi huanza kwa kuwaleta pamoja wanawake wenye umri mdogo, hatimaye huwaingiza wanawake wote ambao sauti zao zinapaswa kusikika, wakiwemo wanawake wenye umri mkubwa zaidi, wanaume, na wale ambao wajibu wao unagusa afya ya mama na mtoto. Kikundi kinachozaliwa hujulikana kama  Kikundi  cha Kujifunza na  Utendaji Shirikishi  (Participatory Learning & Action Group)


Vikundi  vya Kujifunza na  Utendaji Shirikishi  (Tushikamane Groups)

Vikundi vya Kujifunza na Utendaji Shirikishi au Vikundi vya Tushikamane vitajaribu kupunguza  vifo vya akinamama na watoto kwa kutoa nafasi ya mijadala mahali ambapo wanajamii na hususan wanawake, hupewa fursa sawa kuchangia na kutoa mawazo yao, na kuweza kubainisha vipaumbele miongoni mwa  matatizo yote yanayosababisha  vifo.

Njia hii itaelekeza katika utambuzi wa mahitaji  ya jamii na ufumbuzi wake kutoka kwa jamii yenyewe, ufumbuzi ambao utazingatia mambo mengi - zaidi ya afya; yakiwemo kushughulikia  elimu, usafirishaji, maji, huduma ya vyoo na usafi wa mazingira, chakula, agronomia (sayansi mseto ya kilimo bora cha mazao  sambamba na utunzaji wa afya ya udongo), uzazi wa mpango na umasikini( kama ambavyo miradi yenye mafanikio makubwa kama ile inayoendeshwa na Shirika la  Hands 4 Africa  tayari imeonesha!).

Mtandao mpana wa kusaidiana wa Tushikamane, baada ya hapo, unaweza kuisaidia jamii kubuni, kutekeleza na kutathmini njia za ufumbuzi  zinazofaa    ambazo zimetokana na jamii yenyewe. Iwapo kila mmoja atafanya kadri ya uwezo wake, lakini kwa kushirikiana na mtandao mzima, washirika, wakala wa kujitolea, na juhudi mbalimbali ndani na nje, jamii ya Tunguli inaweza kufanikisha juhudi  zao za kutatua matatizo yanayoikabili, wakitumia  njia au mbinu  endelevu ambazo wamezichagua baada ya kuzijadili  kwa makini na  kuzitekeleza vizuri. Kwa mfano  kampeni ya kukuza unyonyeshaji wa maziwa ya mama; chati za maendeleo ya mtoto; mifumo ya vyoo na usafi wa mazingira; huduma ya chanjo ; visima vilivyofunikwa; huduma ya usafiri wakati wa dharura yenye gharama nafuu; uzazi wa mpango; kilimo cha mazao ya chakula na biashara; kuzuia malaria; kuzuia upungufu wa wekundu wa damu (anemia); mafunzo kwa wakunga wa jadi; vikundi vya elimu ya wanawake; nk.

Vikundi vya Tushikamane huanza na wanawake wenye  umri wa uzazi (16-49). Wajawazito, akinamama vijana na wasichana katika umri wa balehe watapewa hamasa ya kipekee kuhudhuria. Kadri muda unavyokwenda, wanajamii wote ambao wanaguswa na masuala ya afya ya mama na watoto wachanga, wakiwemo wanaume, wanawake wenye umri mkubwa zaidi na viongozi wa jamii wataweza kuruhusiwa kuhudhuria na wataeleweshwa kwa nini  vikundi hivi vinawalenga hasa wanawake na watoto.  

Vikundi vya Tushikamane siyo vikundi vya elimu ya afya mahali ambapo mwezeshaji hutoa ujumbe kwa wanakikundi  kama mwalimu. Badala yake, vikundi vya Tushikamane ni fursa ya majadiliano mahali ambapo wanawake na wanajamii hutambua matatizo yao na kuweka vipaumbele, halafu hubuni na kutekeleza njia za ufumbuzi zinazofaa ambazo zimetokana  na jamii yenyewe.

Majadiliano hufanyika kupitia vikao  vya kikundi 14 ambavyo vimewezeshwa vizuri, na katika kila kikao huwa kuna mada mahsusi, na lengo mahsusi. Mikutano hiyo hufanyika kupitia awamu 4. Vikundi vitaongozwa kupitia awamu zote 4, na mzunguko  wa kujifunza  na utendaji shirikishi(PLA), na Wawezeshaji - Ester Paul au Rehema Semwali.

Kama sehemu  muhimu ya ufuatiliaji wa mchakato huu wa kujifunza na utendaji shirikishi, Mradi wa  Tushikamane pia utajaribu kutathmini matokeo ya mradi, kubaini yapi muhimu ambayo tumejifunza  kutokana na mradi kabla ya uwezekano wa kuupanua mradi  siku za usoni. Tathmini hii itasaidiwa  na zoezi lililofanyika hivi karibuni la kuchora  ramani na kukusanya  taarifa za   eneo la mradi, pamoja na kurasimisha majina ya vijiji na vitongoji.




MAELEZO  YA JUMLA JUU  YA MZUNGUKO WA  UTENDAJI WA KIKUNDI CHA  TUSHIKAMANE


Vikundi vya TUSHIKAMANE vitaoongozwa na
Wawezeshaji kupitia mzunguko  wa kujifunza  na utendaji shirikishi   (participatory learning and action cycle) wenye awamu 4 na jumla ya mikutano 14 .




Mchakato   huu wa kikundi cha  Tushikamane huchukua muda gani?
Mchakato wa kuunda kikundi na kuwa timu unaweza  kuchukua takriban miezi 2.  Vikundi vinaweza kukutana takriban kila baada ya wiki 2, na siyo chini ya kila mwezi, kutegemea na utaratibu unaokubalika zaidi kwao. Utekelezaji wa mikakati itakayokuwa imebainishwa unaweza kuchukua kati ya miezi 2 hadi 6. Hivyo, unaweza kutarajia ratiba ifuatayo kwa ajili ya utekelezaji wa mpango huu wa Tushikamane:

Uundaaji kikundi na kujenga timu
Miezi 2 – 4
Awamu1: Utambuzi wa pamoja wa matatizo
Mikutano 5
Miezi 2.5 – 5
Awamu  2: Utambuzi wa pamoja wa njia za ufumbuzi
Mikutano 3
Miezi 1.5 – 3
Awamu 3: Utekelezaji wa pamoja wa  njia za ufumbuzi
Mikutano 3
Miezi 1.5 – 3
Utekelezaji wa njia za ufumbuzi
Miezi 3 – 6
Awamu 4: Kufanya tathmini pamoja
Mikutano 3
Miezi 1.5 – 3
Jumla
Miezi 12 – 24


Hadi hapo tumesema nini?

Maelezo  ya jumla ya mradi wa  Tushikamane:
Tutazishirikisha jamii kwa ukamilifu.
Tutazishirikisha kwa kuunda Kikundi  katika kila kitongoji.
Sehemu zingine, kila kikundi kimeitwa ‘Kikundi cha Kujifunza  na Utendaji Shirikishi  kwa ajili ya Afya ya Mama na Mtoto’. Katika Mradi wa Tunguli, kitaitwa Kikundi cha TUSHIKAMANE( Mkutano wa Kufanya kazi Pamoja au Mkusanyiko wa Uwezeshaji). Kila kikundi kitapitia mzunguko wa mikutano 14 ambayo imeandaliwa kwa ajili ya kuiwezesha jamii kuamua  shughuli gani muhimu zitapewa kipaumbele katika kupunguza vifo vya akinamama na watoto wachanga



Kuanzisha Vikundi vya Tushikamane  – kujitayarisha kuanza


Kuwashawishi  wanajamii  wanaostahili kuhudhuria
Watu ambao wanaathiriwa zaidi  na tatizo wanapaswa kushirikishwa katika uchambuzi wa hali inayowaathiri  na kufanya uamuzi wa nini kifanyike.  Kwa hivyo, RS na  EP watahamasisha wanawake walio katika umri wa uzazi kuhakikisha wanajiunga  na vikundi hivi. Wanawake hao wenyewe ndiyo watakaoamua juu ya uanachama katika kikundi.

RS na EP watawahimiza kutoa kipaumbele kwa wajawazito na mama wenye umri mdogo, pamoja na wanawake walioolewa na wasichana balehe, hasa akinamama na wasichana balehe kutoka katika kaya zenye hali duni zaidi.

Tutawataka waruhusu  mwanajamii yoyote yule ambaye anaguswa na vifo vya akinamama na watoto.  Tunataka hatimaye wanachama wa kikundi wajumuishe wale wote wanaowahudumia  akinamama na watoto kupitia ujauzito, kujifungua na baada ya kujifungua. Hii inaweza kujumuisha, mathalan, wakunga wasaidizi; wafanyakazi wa afya vijijini; viongozi wa jamii wa eneo husika; wafanyakazi wa mashirika yasiyo ya kiserikali au wafanyakazi wa ugani au kwenye miradi ya serikali katika eneo hilo; nk

Ester & Rehema watawashawishi wote kuhudhuria vikundi hivi ambavyo vinaanzishwa.Watahakikisha kuwa wanakikundi wote wnatambua kuwa wajibu wao katika kikundi utakuwa ni kusikiliza na kuheshimu maoni na mawazo ya wanakikundi wakike, halafu kutoa ushauri na msaada pale panapostahili ili kufanikisha lengo la kuboresha afya ya mama na watoto.

Mwenyekiti wa Kikundi na Kamati

Kila kikundi kinaweza kuamua kuchagua kamati  na, au  kutoa majukumu mahsusi kwa baadhi ya wanakikundi. Kamati ijumuishe hasa wanawake-robo tu ndiyo wawe wanaume. Kamati zichague mwenyekiti, na katibu mwanzoni kabisa.

Mwenyekiti anapaswa kuwa mwanamke. Wajibu wa Mwenyekiti ni kukiongoza kikundi. Wajibu huu unajumwisha kuongoza shughuli za kikundi na kutoa dira, kuwasimamia wanakamati na wanakikundi na kukiwakilisha kikundi kwenye mikutano au shughuli zinazostahili katika ngazi ya jamii, wilaya na kitaifa . 

Wajibu wa Katibu ni kuchukua na kutunza kumbukumbu za shughuli za kikundi. Hii inajumuisha kujaza kitabu cha mahudhurio na kuandaa taarifa ya mkutano kila baada ya mkutano kufanyika.
Kadri kikundi kitakvyokua kinakua, kutahitajika kuwepo mweka hazina, wajibu wake ukiwa ni kufuatilia fedha za kikundi na rasilimali zingine za kikundi. 

Wajumbe wa Kamati wote wana wajibu wa kuwashawishi wanajamii kujiunga na Kikundi , na kushiriki katika mikutano. Wajumbe wa Kamati pia wana wajibu wa kuwasaidia  Wawezeshaji (Rehema au Ester) wakati wa mikutano.


Wanajamii wangapi wanatakiwa kuandikishwa kwenye Kikundi?

Idadi kuu ya wanakikundi waliosajiliwa inatakiwa kuwa takriban  50.  Uanachama ni wazi na hivyo inawezekana idadi kuu ya wanakikundi ikaongezeka katika uhai wa kikundi. 

Hata hivyo, siyo wanakikundi wote waliosajiliwa wataweza kuhudhuria kila mkutano wa kikundi. Kuhakikisha ushiriki wa kiwango cha juu, idadi ya wanakikundi waliosajiliwa katika kila kikao inapaswa kuwa kati ya  25-30.  Kukiwa na zaidi ya idadi hii, inakuwa vigumu kwa kila mjumbe kushiriki na mwezeshaji kumudu kikundi. Mikutano inastahili kuhudhuriwa angalau na wanakikundi   10 ili iweze kuwa na tija.  Kama idadi ndogo ya hapo itahudhuria, mwezeshaji na wanakikundi waliopo wanaweza kuzunguka kwenye kaya na kuwaleta washiriki wengine. Kama idadi ya wahudhuriaji ni  ndogo sana, ni bora kuahirisha mkutano na kuandaa kwa ajili ya tarehe nyingine.

Hali halisi na  takwimu kuhusiana na  ukubwa wa vikundi katika maeneo ya vijijini Tanzania

Ushahidi unaonesha kuwa vikundi hufanikiwa zaidi pale angalau asilimia 30 wanakikundi wanakuwa  wajawazito. Kutokana na takwimu za Sensa ya Tanzania, tuliweza kukokotoa na kufanya makadirio juu ya ukubwa wa kikundi:

Nchini Tanzania kuna mfumo rasmi wa vijiji na vitongoji. Kitongoji kina kaya 100.  Kijiji kina vitongoji   3-4 . Kama kikundi kimoja kitahudumia mathalan watu 700 , basi katika maeneo ya vijijini Tanzania hii ingemaanisha:

·              Kitongoji kimoja kina watu takriban  700, ( watu  7 katika kila kaya);
·              hii inafunika takriban eneo la kilomita  6 x 4, (kama  kipimo cha idadi ya watu kwa eneo ni  watu  31 kwa kila eneo la mraba wa kilomita moja; 
·               (ambapo angalau thelusi tatu ya akinamama wanapaswa kuwemo katika kikundi); 
·              Huenda kukawa na wanawake walio katika umri wa uzazi  175 , (kwa sababu hujumuisha robo ya idadi ya watu) 
·              Wenye afya ambao baadhi yao huendelea kupata watoto zaidi ya 6 (idadi ya watoto kwa kila mwanamke 6.3)
·              Kwa kiwango cha vifo vya akinamama  cha mwanamke  1  kwa kila wanwake  200 wanaojifungua kote nchini Tanzania , na huenda kifo cha mwanamke  1 kwa kila  100-150 wanaojifunguakwenye maeneo ya vijijini, kunakuwa na kifo 1 cha mwanamke kila miaka 5 katika kila kitongoji/au kikundi cha wanawake;
·              Kila kitongoji chenye watu  700 kinaweza kupata vizazi   28 mwaka,  (Makadirio ghafi  ya vizazi  39); 
·              Kati ya hao, huenda  watoto wachanga 2 chini ya umri wa  mwezi mmoja  na mmoja zaidi chini ya miaka 5 watakufa kila mwaka katika kila kitongoji.  

Kukiwa na mwezeshaji mmoja akihuhudumia vitongoji 3, atakuwa akihudumia takriban  watu 2,000. Hii inaweza kumaanisha kuwa kila mwezeshaji ataanza  akiwa   na jukumu   la kuepusha  angalau kifo cha mama mmoja kila takriban miaka 2, na karibia vifo vya watoto  7 kila mwaka. Hii  ni changamoto kubwa  kwa mradi au afua yoyote ile.

Kuhakikisha makundi ambayo tayari yapo kwenye  jamii yanashirikishwa

RS na  EP watahitaji kujua ni shughuli gani ambazo mashirika mengine na jamii tayari zinatekeleza au zimepanga. Hii ni muhimu kuhakikisha kwamba hakuna kurudia shughuli  ambazo tayari zimeazishwa  na pia kwamba mipango yote inasabihiana au kuimarisha  shughuli ambazo zinaendelea. Kama tayari kuna vikundi kwenye jamii ambavyo vinatoa huduma, na ambavyo mnaweza kushirikiana, basi vinapaswa kualikwa, wakati mwafaka, kutuma uwakilishi kwenye kikundi cha Tushikamane kinachoanzishwa.

Ester na  Rehena wanapaswa kukutana na  
·         Wenyeviti wa Vijiji;
·         Mashirika ya ngazi za wilaya, kama vile mashirika yanayotoa  misaada na mashirika yasiyo ya kiserikali;
·         Maafisa wa serikali na juhudi zingine za kiserikali;
·         wabia wengine wowote ili kupata taarifa juu ya vikundi vingine vilivyopo.

Kikundi cha  Tushikamane kitakuwa na uhai wake wa pekee, lakini kinalazimika kufanya kazi kwa maelewano na  ushirikiano na juhudi na vikundi vingine vilivyopo  kwenye jamii.


Mara baada ya vikundi kuanzishwa …

Mara baada ya vikundi   vya Tushikamane kuanzishwa  kwa ukamilifu, vinahitaji kuanzisha mchakato wa kujadili na kutambua masuala gani yanayosababisha vifo vya mama na watoto wachanga  ambayo yanapaswa kupewa kipaumbele. Mijadala hii inapaswa kufanyika kupitia mfululizo wa mikutano 14 itakayoandaliwa  na Rehena na Ester, chini ya uongozi na  usimamizi wa  Alex Gongwe; na kuwezeshwa  na  Wilbard Mrase na Mchungaji  Isaac Mgego.

Mwishoni wa mikutano 14, kutakuwa na tathmini rasmi ambayo itapima ufanisi wa mchakato mzima.Kama mchakato umekwenda vizuri, mchakato mwingine wa mikutano 14 utaanza tena kutafuta vipaumbele vipya. Kwa sababu hii mchakato huu hujulikana kama Mzunguko wa Kujifunza na Utendaji  Shirikishi (‘PLA Group Cycle’).



MZUNGUKO WA UTENDAJI WA  KIKUNDI CHA TUSHIKAMANE
Awamu ya  1: kubaini matatizo pamoja
Shabaha ya Awamu 1 ya mzunguko  wa mikutano ni Kikundi kubainisha matatizo ya afya ya mama na watoto wachanga ambayo yatapewa kipaumbele




Yafuatayo ni maelezo ya jumla juu ya  mikutano 14. Maelezo yake kwa kirefu yatatolewa kwenye Kiongozi cha Mafunzo.



Mkutano  wa 1: Kukiandaa kikundi kuanza kazi


Malengo ya mkutano ni:
·         Kuutambulisha mpango katika mazingira ya jamii husika
·         Kutambulisha utaratibu wa ‘kujifunza na utendaji shirikishi’  (‘Participatory Learning and Action’)
·         Kuunda kamati ya kikundi na kuweka sheria za kuwaongoza wanakikundi


Mkutano  wa 2: Kubaini matatizo ya afya yanayowakumba  akinamama


Lengo la mkutano ni :
·         Kujadili  hali halisi ya matunzo ya nyumbani ya mama waliojifungua na mienendo yao katika kutafuta huduma zinazostahili
·         Kubaini matatizo ya kiafya yanayowakumba wanawake wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua

Mijadala katika mikutano ya vikundi itachochewa na Rehena na Ester kwa kutumia zana maalum ambazo zimeandaliwa  kwa ajili ya lengo hilo– mathalan  kadi za picha ambazo zinaonesha matatizo ya akinamama na watoto wachanga chini ya wiki 4, mambo yanayochangia, na njia za kuzuia au kudhibiti matatizo hayo ya kawaida.

Kuna jumla ya kadi  60 :
·         Kadi za matatizo(kadi 21): zinaonesha matatizo makubwa ya kiafya ambayo yanawakabili  akinamama na watoto wachanga chini ya wiki 4
·         Kadi za mambo yanayochangia ( kadi 17): zinaonesha mambo muhimu ambayo yanachangia matatizo hayo.
·         Kadi za shughuli za uzuiaji wa matatizo hayo (kadi 13 ): zinaonesha shughuli muhimu ambazo watu wanaweza kufanya ili kuzuia matatizo yanayowakumba akinamama na watoto wachanga kutokea.
·         Kadi za shughuli za usimamizi wa huduma  (kadi 9 ): zikionesha shughuli muhimu ambazo watu wanaweza kufanya kupambana na matatizo ambayo huwakumba akinamama na watoto wachanga pale yanapoibuka
















Mkutano wa 3: Kubaini matatizo yanayowakumba watoto wachanga chini ya wiki 4


Malengo ya mkutano ni kubaini matatizo yanayowakumba watoto wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua; kujadili hali halisi ya matunzo ya watoto wachanga chini ya wiki 4 nyumbani; na kujadili kwa nini, lini na jinsi gani wanawake  hutafuta msaada.


Mkutano wa  4: Kuweka vipaumbele

Lengo la mkutano huu ni kubaini matatizo makubwa 3 kwa  afya ya akinamama na watoto wachanga ambayo yatapewa kipaumbele katika mzunguko  huu.


Mkutano wa  5: Kubaini mambo yanayochangia

Lengo la mkutano ni kubaini visababishi vya matatizo makubwa ambayo yameamuliwa kupewa kipaumbele




MZUNGUKO WA UTENDAJI WA KIKUNDI CHA TUSHIKAMANE
 Awamu ya  2: Kubaini pamoja  ufumbuzi.
Shabaha ya Awamu ya 2 ya mzunguko wa mikutano ya Kikundi ni  kupanga ufumbuzi wa matatizo yanayowakumba akinamama na watoto wachanga





Mkutano wa  6: Kubaini shughuli za uzuiaji na usimamizi  wa matatizo

Malengo ya mkutano ni:
·         Kubaini shughuli ambazo zinaweza kuzuia matatizo makubwa yanayowakumba akinamama na watoto kutokea.
·         Kubaini shughuli  kwa ajili ya usimamizi wa matatizo makubwa ya afya ya akinamama na watoto wachanga chini ya wiki 4 kama tayari yapo


Mkutano wa 7: Kubaini ufumbuzi

Malengo ya mkutano ni:
·         Kubaini njia za ufumbuzi kwa ajili ya kuzuia na kusimamia matatizo yaliyopewa kipaumbele.
·         Kubaini rasilimali au nyenzo ambazo zinaweza kusaidia na vikwazo ambavyo vinaweza kuzuia utekelezaji wa njia za ufumbuzi. (mathalan makundi yote 2-wafanyakazi wa afya vijijini na wakunga wasaidizi wanaweza kusaidia kufanikisha masuala mbalimbali kama vile unyonyeshaji,uzazi wa mpango; chanjo; usafi; uzuiaji malaria; na utambuzi wa dalili za  ugonjwa kali.)


Kutokana na uzoefu, njia nyingi za kawaida za  ufumbuzi wa matatizo zinazobainishwa na vikundi ni pamoja na:
·         Elimu ya afya
·         Usafiri
·         Mfuko wa  kikundi  wa akiba
·         Vifaa safi kwa ajili ya kujifungua
·         Shughuli za kuongeza pato
·         Mafunzo kwa wakunga wa jadi
·         Kushirikiana na ushawishi kwa vituo vya kutolea huduma za afya
·         Bustani za mbogamboga

Baada ya Mkutano wa 7, wanakikundi wanapaswa kukutana kwa ajili ya kuandaa na kufanya mazoezi ya mrejesho kwa jamii katika kikao kinachofuata.


Mkutano wa  8: Kutoa mrejesho juu ya maendeleo ya mikutano  kwa jamii

Malengo ya mkutano ni :
·         Kutoa mrejesho kutokana na  mijadala kwa wanajamii wote, ikijumuisha matatizo ambayo imeamuliwa yapewe kipaumbele na ufumbuzi wake.
·         Kukusanya mawazo na maoni ya wanajamii wote juu ya masuala mbalimbali yaliyojadiliwa na  kikundi.
·         Kupata msaada wa hali na mali  kutoka kwa wanajamii wote kwa ajili ya utekelezaji wa njia za ufumbuzi zilizobainishwa.





MZUNGUKO WA UTENDAJI WA KIKUNDI CHA TUSHIKAMANE
Awamu ya 3: Kutekeleza kwa pamoja njia za ufumbuzi
Shabaha ya Awamu ya 3 ya mzunguko wa mikutano ni Kikundi kiweze kutekeleza njia za ufumbuzi zilizobainishwa ili kukabiliana na matatizo ya afya ya akinamama na watoto  wachanga.






Mkutano wa  9: Kupanga njia za ufumbuzi

Malengo ya mkutano ni:
·         Kupata ushirikiano na maelewano kutoka kwa wadau wote kuhusiana na njia za ufumbuzi zilizopendekezwa
·         Kukamilisha na kuuafiki  mpangokazi kwa ajili ya njia za ufumbuzi .

Mkutano wa  10: Kukusanya rasilimali

Lengo la mkutano ni kupanga jinsi ya kukusanya rasilimali ambazo zinahitajika kwa ajili ya utekelezaji wa njia za ufumbuzi.

Ukusanyaji rasilimali

Baada ya Mkutano wa 10 wanakikundi wanapaswa kuanza utafutaji na ukusanyaji wa rasilimali mbalimbali kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za ufumbuzi.

Mkutano wa 11: Kuandaa zana za ufuatiliaji

Lengo la mkutano ni kupanga jinsi ya kufuatilia maendeleo ya utekelezaji wa shughuli za ufumbuzi.

Utekelezaji na ufuatiliaji wa shughuli za ufumbuzi
Baada ya Mkutano wa  11, wanakikundi wanapaswa kutekeleza na kufuatilia shughuli zao za ufumbuzi. Wanatakiwa kuifanya  kazi hii kwa kipindi cha miezi 3 hadi 6. Vikundi na vikosikazi  wakutane mara kwa mara na mwezeshaji wao katika kipindi hiki, kupitia maendeleo ya utekelezaji, kusherekea mafanikio na kubaini na kuzifanyia kazi changamoto zozote. Ratiba ya kufanyika kwa mikutano itaamuliwa na wanakikundi wenyewe.



MZUNGUKO WA UTENDAJI WA KIKUNDI CHA TUSHIKAMANE
 Awamu 4: Kutathmini pamoja

Shabaha ya Awamu ya  4 ya mzunguko wa mikutano na kutathmini matokeo ya shughuli za ufumbuzi ambazo zimetekelezwa juu ya matatizo ya akinamama na watoto wachanga yaliyobainishwa.



           
Mkutano wa  12: Kuandaa kutathmini

Malengo ya mkutano ni:
·         Kuchunguza kwa nini kutathmini pamoja  kikundi na shughuli za ufumbuzi ni muhimu.
·         Kujiandaa na kupanga kwa ajili ya zoezi la tathmini

Kukusanya data kwa ajili ya tathmini

Baada ya Mkutano wa  12, wanakikundi wanapaswa kwa pamoja kukusanya data wanazohitaji kwa ajili ya tathmini.

Mkutano wa  13: Kutathmini matokeo ya shughuli za ufumbuzi juu ya matatizo yaliyopewa kipaumbele

Malengo ya mkutano ni:
·         Kutathmini kwa kiwango gani cha ufanisi matatizo yaliyopewa kipaumbele yameshughulikiwa
·         Kutathmini utendaji wa Kikundi
·         Kupanga kwa ajili ya wakati ujao.

Mkutano wa 14: Kupanga kwa ajili ya wakati ujao  
  
Lengo la mkutano ni kuamua Kikundi kifanye nini baada ya hapo.

Anza upya mzunguko wa utendaji
Baada ya Mkutano wa  14, Kikundi kinapaswa kuwezeshwa kuanzisha tena mzunguko  katika  Awamu ya  1, 2 au  3 kutegemea na kipi kilijadiliwa na kuamuliwa katika mkutano.
Baada ya mzunguko 1 wa mikutano ya kikundi, Kikundi kinapaswa kujisikia kuwa kinaimiliki  programu na kuwa na uwezo wa kuendelea kukutana. Wajibu wa wasimamizi na viongozi ni kuwepo kwa ajili ya kuendelea kutoa ushauri wa kitaalam, lakini dira na shabaha ya kikundi viamuliwe na wanakikundi wenyewe.



No comments:

Post a Comment